Je, wewe unafahamu nini kuhusiana na Imani ya Mitume (inayounganisha wakristo Ulimwenguni mwote) ambayo Wakristo wengi ulimwenguni huungana pamoja katika kuikiri? Katika makala hii tutajifunza kwa ufupi juu ya Imani ya Mitume. Ni matumaini yangu kuwa makala hii itakufungua angalau kidogo katika kuifahamu Imani ya Mitume, na kuungana na Wakristo wengine katika kuikiri.
Kanuni za Kiimani
Tangu kuanzishwa kwa Kanisa, Wakristo walitengeneza miuhtasari
mifupi na rahisi ya imani. Mihutasari hii mifupi ilijulikana kama hihtasari ama
kanuni za imani. Mojawapo ya Mihtasari hii mifupi ni Imani ya Mitume. Watu walipokuwa
wakijiandaa kwa ubatizo katika karne za mwanzo za Kanisa la Kikristo
walijifunza muhtasari mfupi wa kile ambacho Wakristo wote walikiamini. Mojawapo
ya mihtasari hii ya Imani ni Imani ya Mitume ambayo ilikubalika na kupokelewa
kwa upana katika kanisa, kwasababu ilionekana kuwa na mafundisho muhimu kutoka kwa wale mitume 12
waliokuwa wafuasi wa kwanza wa Yesu. Ilikuwa ni katika imani ya mitume Wakristo
walikiri kupokea ubatizo katika Kristo. Imani ya Mitume ni muhtasari wa kile
Kanisa linafundisha, na kile ambacho Wakristo kwa pamoja wanaamini.
Imani ya Mitume
Namwamini Mungu Baba mwenyezi, muumba mbingu na nchi:
Na Yesu Kristo Mwana wake pekee, Bwana wetu, aliyechukuliwa
mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, akazaliwa na bikira Mariamu, akateswa zamani
za Pontio Pilato, akasulubiwa, akafa, akazikwa, akashuka mahali pa wafu; siku
ya tatu akafufuka, akapaa mbinguni, ameketi mkono wa kuume wa Mungu Baba Mwenyezi, kutoka huko atakuja kuwahukumu
walio hai na watu wafu.
Namwamini Roho Mtakatifu; na kanisa takatifu ya Waamini
wote; na ushirika wa watakatifu; na ondoleo la dhambi; na kiyama ya mwili; na
uzima wa milele.
Amina.
Chanzo cha Imani ya
Mitume
Wakati fulani iliaminiwa na kufundishwa kwamba Imani ya
Mitume iliandikwa katika kipindi cha karne ya kwanza na mitume kumi na wawili
wenyewe. Hata hivyo iliaminika pia kuwa kila mtume alichangiwa wazo lake la
kitheolojia katika maneno yaliyomo katika Imani ya Mitume. Lakini ukweli ni
kwamba hakuna udhibitisho wala ushahidi wowote katika historia unaoonyesha kuwa
Mitume walihusika kwa njia moja ama nyingine katika kuunda ama kuandaa Imani hii
ya Mitume ambayo tunaungana na wakristo wote Ulimwenguni kuikiri. Kama mitume
hawakuandika Imani hii ya mitume ni nani alihusika? Ni ngumu kusema ni nani
aliandika kwa sababu hakuna mwandishi aliyejitokeza kudhibitisha kuwa yeye ndio
mwandishi halali/halisi.
Wapo ambao waliamini kuwa Imani hii ya Mitume ilianza na
maswali ambayo wakristo walikua wakiulizwa wakati wa kupata ubatizo au kukiri
kile wanachokiamini. Mfano ‘unaamini katika Mungu Baba aliyeumba Mbingu na nchi?
Je, unaamini kuwa Kristo alichukuliwa mimba kwa uweza wa Roho mtakatifu na
kuzaliwa na bikira Maria’ nk.
Katika karne ya kwanza na ya pili, huenda ikawa kila
kutaniko la kanisa lilikuwa na taratibu zake za kiimani, au njia ya kufupisha
ukweli muhimu wa Biblia kwa wale ambao hawakuwa na uwezo wa kusoma ama kuielewa
Biblia kwa kina. Sio watu wote walikua na uwezo wa kuelewa ama kustaimili yale
yaliyokuwa kwenye Biblia kwa kipindi kichyo. Lakini kufikia karne ya tatu au ya
nne, misingi ama taratibu fulani za kiimani zilikuwa zikizidi kuwa maarufu
zaidi na kutumika katika makanisa mengi.
Taratibu ama Imani mojawapo ambayo ilijivunia umaarufu kwa
njia hii ilikuwa ni imani ya kanisa la Roma, Imani ambayo ilitambulika kwa jina
la Imani ya Roma. Imani hii inafanana sana na Imani ya Mitume na ilipelekea wasomi
wengi kuamini kuwa Imani ya Mitume ilikua ni toleo la baadaye baada ya Imani
hii ya Roma. Ukweli ni kwamba Imani ya mitume haikutokana na Imani ya Roma,
bali ilianzia katika kanisa la kwanza la Kristo.
Kusudi la kuundwa kwa
Imani ya Mitume
Imani ya mitume iliundwa ili kuwawezesha wakristo kuwa
waaminifu na neon la Mungu na kuendelea kusimama katika kweli ya Mungu na kuwa
na umoja katika kanisa la Kristo Bwana wetu. Iliundwa ili kuwasaidia watu kupata muhtasari
wa Neno la Mungu na kuwa na uwezo wa haraka katika kuishika kweli ya Kristo na
kuepuka udanganyifu ambao ungeweza kuingizwa katika kanisa na waalimu wa uongo.
Mkristo atambue nini
katika neno la Mungu pamoja na Imani ya Mitume?
Kuwa wakati kwa nia njema tunaweza kuchukulia kanuni fulani
za imani kuwa ni sawa na neno la Mungu (Biblia). Japo tunaikiri Imani ya
Mitume, ni lazima kuelewa kuwa maandiko matakatifu ni neno la Kristo na ndilo
lenye mamlaka juu ya vitu vingine vyote, na ndilo chanzo cha mafundisho yote ya
kweli. Tusije tukalisahau neno la Kristo na kushikamana na tamaduni zetu ndani
ya Kanisa. Hakuna tamaduni au imani inayopaswa kuinuliwa au kulinganishwa na
neno la Mungu. Biblia pekee ndio chanzo na msingi wetu katika Imani. Tamaduni
za Imani kama Imani ya Mitume ni zana ya kufundishia na kutoa muhtasari wa
uelewa wetu wa Maandiko.
Imani ya Mitume
inatusaidia vipi sisi Wakristo katika Imani yetu?
Kama tulivyoona, hakuna kanuni ama tamaduni ya imani inayoweza
kuchukua nafasi ya Maandiko. Lakini hii haimaanishi kwamba kanuni ama taratibu
za imani hazina nafasi katika maisha ya Kikristo. Imani ya Mitume ni zana
inayotoa kanuni na taratibu kwa watu wa Mungu. Moja ya kazi muhimu ya Imani ya
Mitume, kama kanuni zote za kiimani, ni kulisaidia kanisa katika kujua ukweli
juu ya Mungu, kurekebisha mafundisho ya uongo ambayo yanaweza kuingizwa ndani
ya kanisa, kufundisha na kuandaa waumini wapya kwa uaminifu na ukomavu katika
imani ya kanisa. Pia inatuongoza na kutusaidia katika kumwabudu Mungu na
kuikiri Imani, na zaidi ya yote ni kutoa muhtasari wa Imani ya Mkristo na kuliweka
kanisa la Kristo katika umoja.
Imani ya Mitume inatukumbusha ukweli uliopo ndani ya imani
yetu, kufafanua ufunuo wa Biblia juu ya Yesu Kristo, na kazi Kristo katika
ukombozi wetu. Kanisa linategemea mukhtasari mfupi wa imani katika kuungama
pamoja na kueneza Ukristo wa kweli ulimwenguni kote.
Hitimisho:
Katika haya tuliojifunza juu ya Imani ya Mitume, na wakati
ulimwengu ukiendelea kuchanganikiwa na kuliacha neno la Mungu, ni muhimu kwa
wakristo wote kusimama Imara katika Maandiko na kuijua kwa kina kweli ya Mungu
ili kuepuka mafundisho na Imani za uongo ambazo zinaendelea kuzaliwa siku hadi
siku. Mababa wa kanisa walielewa ukweli huu, ndiyo maana walifanya kazi kwa
bidii ili kulitolea kanisa muhtasari wa uaminifu wa mafundisho ya Maandiko,
kama Imani ya Mitume.
Kwasababu ya Kalvari mimi nimewekwa Huru,
Rumishael Ulomi
Copyright © www.kilicentric.com
